Rais wa Gambia Yahya Jammeh, amesitisha utekelezaji wa adhabu ya kifo kwa wafungwa waliohukumiwa dhabu hiyo.
Ofisi ya rais huyo imesema hatua hiyo inafuatia
wito wa kimataifa uliotaka adhabu hiyo ikomeshwe lakini ameonya kuwa
usitishaji huo ni wa muda.
''Hatua
itakayofuata itatategemeana na iwapo kiwango cha uhalifu kitapungua
ambako usitishaji huo utakuwa wa moja kwa moja, na iwapo uhalifu
utaongezeka basi hukumu hizo zitatekelezwa,'' taarifa ya rais huyo
imesema, kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters.
Kiongozi huyo wa Gambia alikosolewa na jumuiya ya kimataifa mwezi uliopita alipotangaza kutekeleza adhabu ya kifo kwa wafungwa.
Wafungwa tisa waliuawa kwa kupigwa risasi
kufuatia uamuzi wa rais huyo huku wengine 37 wakibakia katika orodha ya
wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kifo.
Rais huyo alisema kuwa wafungwa wote arobaini na
saba waliohukumiwa adhabu ya kifo wangekuwa wamekwishauawa kufikia
katikati ya mwezi Septemba mwaka huu.
Utekelezaji huo wa hukumu ya kifo ulikuwa ni wa
kwanza nchini Gambia iliyo maarufu kwa watalii, katika kipindi cha miaka
27, huku wanaharakati wa haki za binadamu wakisema kuwa wengi wa
wafungwa hao ni wale wa kisiasa.
Umoja wa Afrika na mashirika ya kutetea haki za binadamu walipinga adhabu hiyo.
Benin ambayo ni mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa
Afrika ilimtuma waziri wake wa mambo ya nje kwenda nchini Gambia
kumuonya Bwana Jammeh kuacha kutekeleza adhabu ya kifo kwa wafungwa hao.
Siku ya Ijumaa kundi la Upinzani la Gambia
liliiambia BBC kuwa lina mpango wa kuanzisha serikali likiwa uhamishoni
katika nchi jirani ya Senegal katika kipindi cha siku chache zijazo.
Lengo la kundi hilo la National Transitional
Council of The Gambia (CNTG) ni kuona linamaliza utawala wa ki-dikteta
wa rais Yahya Jammeh.
Hukumu ya kifo ilifutwa wakati wa utawala wa
rais wa zamani wa nchi hiyo Dawda Jawara lakini ikarejeshwa tena muda
mfupi baada ya rais Jammeh kunyakua madaraka mwaka 1994.
No comments:
Post a Comment