BBB

advertisement

tangaza sherehe

ADVERTISEMENT

Tuesday, September 18, 2012

MICHANO: AKINA JB MMEMUONA LUCY KOMBA?


Lucy Komba.

WIKI kadhaa zilizopita nilitumia mistari michache mahali hapa  kumkumbusha mwigizaji Vincent Kigosi ‘Ray’ kuwa Steven Kanumba aliyekuwa akiitangaza tasnia ya filamu kimataifa alikuwa ameondoka hivyo nilitangaza nafasi ya ajira kuwa anahitajika mtu wa kufanya kazi hiyo.
Hakuna mwanaume aliyejitokeza hadi mwigizaji bidada Lucy Komba alipoamua kuchukua jukumu hilo huku akina Jacob Steven ‘JB’ na wenzake wakimkodolea macho.
Lucy Komba ni mwigizaji ‘legendary’. Namjua akiwa shule ya msingi pale Oysterbay na sekondari kule Kibosho, Kilimanjaro. Nilimuona akisomea Diploma ya Information Technology (IT), Dar kabla ya kuonekana kwenye tamthiliya kadha wa kadha runingani zikiwemo Radi, Zizimo, Sayari, Gharika na Tufani.
  Baada ya marehemu Kanumba kufungua njia, mwanadada Lucy  aliyezaliwa Oktoba 24, 1980 akaona ndipo mahali pekee pa kuchomoka kimataifa kwani ungemwambia nini kwa soko la nyumbani wakati kupitia kampuni yake ya Poyaga Productions ameshatengeneza na kusambaza mwenyewe zaidi ya sinema 20 hivyo ana uzoefu wa kutosha.
Habari njema ni kwamba dada huyo amepata mkataba wa makubaliano ya kufanya filamu na aliyekuwa meneja wa kimataifa wa marehemu Kanumba, Richard Nwaobi ambaye pia ni meneja wa mwigizaji Rose Ndauka.
Mwanzoni mwa mwaka huu, Lucy akiwa ni mfanyakazi wa serikalini katika Mahakama Kuu, alipaa na kwenda kufanya kazi na waigizaji wakubwa ndani na nje ya Bara la Afrika huko nchini Ghana akiwa kashikwa mkono na marehemu Kanumba.
Katika mazungumzo yangu na Lucy aliniambia: “Unajua nilipokwenda Ghana na Kanumba, nilipata nafasi ya kufanya filamu nyingine nchini Searra Leone inayoitwa Repackage Live ambayo imeshakamilika. Itazinduliwa katika nchi zote ambazo washiriki wanatoka.”
Mpaka sasa Lucy ameshafanya filamu mbili za kimataifa akishirikiana na waigizaji wakubwa wa Gollywood, Ghana na Nollywood, Nigeria. Pia wa Sierra Leone.
Katika harakati hizo za kuitangaza tasnia ya filamu za Kibongo, ametokea kwenye jarida kubwa la filamu barani Afrika liitwalo Filmbiz. Katika toleo hilo anaonekana sambamba na mastaa kama Ini Edo na Van Vicker.
Lucy anasema katika kazi zake hizo za kimataifa alilazimika kuwa anaielezea tasnia ya filamu za Kibongo kwa kila nchi aliyokwenda.
Katika kuitangaza tasnia ya filamu za Kibongo kimataifa niliwahi kuandika hapa kuwa ni wazi kwamba baada ya kuondoka kwa Kanumba (Uncle JJ), kazi hiyo itafanywa na waigizaji wa kike. Ukimwacha Lucy, yupo Yvonne-Chery Ngatikwa ‘Monalisa’, Rose Ndauka na Wema Sepetu aliyefanya mazungumzo na mwigizaji mkubwa ndani na nje ya Afrika wa Nollywood, Nigeria, Omotola Jalade. Naamini Lucy na wenzake wameonesha njia kwa waigizaji wa kiume.
Turudi kwa waigizaji wa kiume. Niliamini kuna wasanii ambao wangechukua nafasi ya Kanumba kimataifa wakitajwa akina JB, Ray, Franky Mwikongi, Sajuki na wengine wawili watatu.
Kuna vitu vingi vinavyogonga kuwa ndizo sababu za kushindwa kwao. Elimu ndogo, kutojua lugha ya Kiingereza, mtandao wa kuunganishwa na waigizaji wakubwa, uvivu, kuridhika na filamu zilizo chini ya kiwango wakiamini wanauza leo wasijue kuwa kesho hazitauza, kulewa umaarufu wa ofa za vitu vidogovidogo kutoka kwa matajiri uchwara na mengine yanayofanana na hayo. Nimesomeka. For the love of game!
 

No comments:

Post a Comment

SHARE

TOA MAONI YAKO KUHUSU POST HII

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...