BBB

advertisement

tangaza sherehe

ADVERTISEMENT

Friday, August 17, 2012

MUME: MKE WANGU KANIIBIA NYETI



UNAWEZA usiamini lakini ukweli ni kuwa Juma Ali (48), mkazi wa Mtoni jijini Dar es Salaam amedai kwamba mkewe, Hadija Chande (40) (pichani) amemchezea kishirikina, hivyo kujikuta hana nyeti ya kiume.
Taarifa kutoka katika vyanzo vyetu vya habari zimedai kwamba Ali kwa sasa hana uwezo wa kufanya tendo la ndoa kwa kuwa nyeti yake imetoweka kimiujiza na shutuma zote anambebesha mkewe kwamba ndiye aliyefanya ‘mchezo’ huo.
Habari zinadai kuwa kutokana na hilo, kumezuka mgogoro mkubwa kati ya wanandoa hao kwani mume amekuwa akimdai mkewe  arejeshe nyeti yake, jambo ambalo halijawezekana.
Imedaiwa kuwa Hadija, mara baada ya kufunga ndoa na Ali mwaka 1996 alikuwa na wivu wa kupindukia, hivyo kuamua kutafuta dawa na kumfanyia mumewe ili ndoa yao izidi kuimarika lakini mara baada ya kutenda alichoambiwa afanye kama dawa, nyeti ilitoweka na kubaki na ‘kipande’ kidogo cha kusaidia kutoa haja ndogo.
“Kutokana na madai ya Ali, mkewe aliamua kufungasha virago na kutoweka nyumbani na kwenda kusikojulikana wakati mumewe yupo kazini,” kilisema chanzo.
Gazeti hili baada ya kusikia habari hizo za kushangaza, lilimtafuta Ali ambaye baada ya kuulizwa kuhusu mkasa huo alititirisha maneno kama ifuatavyo:
“Ni kweli hayo uliyoambiwa. Kwa sasa ninachomdai mke wangu aliyetoweka ni nyeti yangu, naomba anirudishie kwani ufumbuzi wa mgogoro wetu hauwezi kupatikana kamwe kama hatazirudisha.
“Hapa unaponiona ndugu mwandishi mimi siyo mwanaume tena. Sina ‘kitu’, hapa kimebaki ‘ kipande’ kama kalamu ambayo haifanyi kazi yoyote. Mke wangu nilipomuoa alinikuta nina watoto sita niliozaa na mke niliyemuacha mwaka 1994, sasa hivi siwezi kufanya tendo la ndoa.
“Mgogoro wa kutoweka na nyeti yangu ulianzia mke wangu alipoanza kunilalamikia kuwa natembea nje ya ndoa na akaniahidi kuwa ni lazima atanidhibiti. Madai yake niliyapinga lakini nguo zangu za ndani zikaanza kupotea. Nilipomuuliza alisema angeninunulia nyingine, nilikuwa na mashaka naye, nikamuomba anirudishie lakini hakufanya hivyo.
“Mara tu chupi zangu zilipoanza kupotea, nikawa sisikii hamu ya tendo la ndoa. Mwezi uliopita, nyeti yangu ikawa imetoweka, nilipomuuliza akawa mbogo. Ilipofika Julai 28, mwaka huu, saa sita mchana, nilitoka kazini na kurudi nyumbani lakini sikumkuta mke wangu na nguo zangu za ndani na soksi hazikuwepo pia.
“Licha ya nguo, picha zangu nazo alizichukua na nilipomuuliza mtoto wangu Karim akasema mama yao amesema kabeba vitu vyake vyote ndani ya nyumba na hakumuambia anakokwenda.
“Nilikaa siku tatu, nikaamua kwenda serikali ya mtaa wetu ya Mtoni na wakanishauri nikaripoti polisi ambako nilipokwenda walifungua jalada namba namba MTG/RB/2054/2012. Polisi waliniambia nitakapomuona popote niwaarifu ili wamkamate.
“Nilisafiri kwenda mikoani na niliporudi nilikuta barua kutoka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) wilayani Temeke ikinitaka niende katika ofisi zao kwa kuwa mke wangu kafungua shauri la kutaka talaka, jambo nililogundua kuwa alishauriwa na rafiki zake ili nimpe nyumba.
“Najua kilichomtoa mke wangu nyumbani ni kushindwa kunirejeshea nyeti yangu, hapa ameshaniua hivyo siyo rahisi kwake kurudi kwani hatafurahia tendo la ndoa. Ili kesi hii iishe sharti ni moja tu kwamba anirudishie nyeti yangu,” alisema Ali.
Mke wa Ali, Hadija alipohojiwa kuhusu sakata hilo alikuwa na haya ya kusema:
“Mbona na mimi sizai na sina hata mtoto wa dawa? Kuhusu kwamba nimetoweka na nyeti yake ni kwamba mimi sijui mambo hayo, asinifuatefuate.”
Mjomba wa Hadija, Abdalah Chande alipoulizwa kuhusu sakata hilo, alikiri kuelezwa na Ali kuhusu mgogoro huo na kudai kuwa alimzushia kuwa yeye ndiye anayemharibu mpwae (Hadija) na akampiga marufuku kukanyaga nyumbani kwake, akaahidi kushirikiana na baba yake mdogo kutatua tatizo hilo.
Baba mdogo wa Hadija  aliyejitambulisha kwa jina moja la Juma alipoulizwa kuhusu mgogoro huo alisema hautambui lakini alimlaumu mwanaye huyo kwa kupeleka shauri hilo Bakwata kabla ya kulifikisha kwake.

  

No comments:

Post a Comment

SHARE

TOA MAONI YAKO KUHUSU POST HII

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...